Mbunge
wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola amesema atawashawishi wananchi
wasikichague Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi Mkuu
utakaofanyika nchini Oktoba mwaka huu ikiwa serikali haitatekeleza
miradi ya kupekeleka maji katika Wilaya ya Bunda mkoani Mara na hasa
jimboni kwake.
Lugola
aliyasema hayo jana, wakati akichangia mjadala kuhusu taarifa ya
utekelezaji ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira na ile ya
Kilimo, Mifugo na Maji baada ya kuwasilishwa bungeni jana.
Alisema
mradi wa ujenzi wa bomba la maji kutoka Tamau hadi Bunda ambao pia
unakusudia kuvipatia maji vijiji vya Bulamba Bizimbwe na Mwisenye
umekuwa kizungumkuti kwa muda mrefu sasa.
Alisema
inasikitisha kwenye kitabu cha taarifa ya Waziri wa Maji, Prof.
Jumanne Magembe haujaweka mradi huo na badala yake ameweka miradi mingi
ya kwenye jimbo lake.
“Na
hata kwenye kitabu hiki cha taarifa yake Mheshimiwa Waziri, Hakuna
mradi huu wa maji ya Bunda, mradi mkubwa, lakini ukienda kwenye miradi
yake ya Same, Mwanga ndiyo imejaa kwenye kitabu hiki, kwa nini
nisiamini unafanya kazi kwa kupendelea maeneo yako, ” alisema Lugola.
Alisema
wakazi wa Bunda wanahitaji maji hayo kutoka Ziwa Victoria lilipo
umbali wa kilometa 20 lakini mpaka sasa ni zaidi ya miaka sita tangu
mradi huo uasisiwe hawajapata.
Alisema
kwa sasa taifa linaelekea kwenye uchaguzi ambao anaamini CCM
kitaendelea kushinda kwa kishindo kwa kuwa Rais Jakaya Kikwete amefanya
mabadiliko ya mawaziri ambayo alitaka sasa yawe ni mabadiliko yenye
tija.
Hata
hivyo alimtaka Maghembe kufanya mabadiliko haraka ya miradi ya maji kwa
kuwa wakazi wa Bunda akiwemo mwenyewe hawatakubali kuipigia CCM kura
ikiwa hawatapata maji mpaka kufikia kwenye uchaguzi huo.
“Mheshimiwa
Maghembe unao muda wa kufanya mabadiliko wananchi wa Bunda
hatutakubali, hatutakubali kupiga kura kwa Chama Cha Mapinduzi, iwe ni
udiwani, wabunge, hata mimi nitasema msinipigie kura, haiwezekani zaidi
ya miaka sita wananchi wanatumia maji taka, mradi umekwama pesa
hakuna,” alisema.
Awali
akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Kamati ya Bunge ya
Kilimo, Mifugo na Maji, Mjumbe wa Kamati hiyo, Said Nkumba alisema
halmashauri nyingi nchini zina madeni makubwa kutoka kwa makandarasi
hivyo akashauri serikali itoe fedha kwa wakati kwa ajili ya utekelezaji
wa miradi hiyo.
Kamati
hiyo pia ilipendekeza serikali kuanza utaratibu wa kutumia mita za
maji kwenye taasisi zake ili kuepukana na tatizo sugu la kutolipia
ankara.
CHANZO: NIPASHE
ConversionConversion EmoticonEmoticon