.

Awekewa mikono ya mtu mwingine India


  • Dar es Salaam. Madaktari katika Chuo cha Tiba cha Amrita, Kochi huko India wamefanikiwa kufanya upasuaji wa aina yake wa kupandikiza mikono mipya kwa binadamu aliyekatika viungo hivyo.
    Upandikizaji huo uliofanyika Januari 12 na 13, ulifanikiwa kwa mara ya kwanza, baada mwanamume mwenye umri wa miaka 30, aliyekatika mikono katika ajali ya treni kuwekewa mingine. Mikono hiyo mipya ilichukuliwa kutoka kwa kijana wa miaka 24 aliyepata aliyefariki katika ajali ya gari.
    Mkuu wa kitengo cha upasuaji katika chuo hicho, Profesa Subramania Iyer alisema: “Siku 14 baada ya upasuaji, mikono ilikubaliwa na mwili na ikaanza kujongea, yaani aliyepandikizwa aliweza kuisogeza huku na kule. Mgonjwa alitolewa chumba cha wagonjwa mahututi na huduma nyingine za kumchunguza ziliendelea.”
    Daktari katika Taasisi ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu Hospitali ya Muhimbili (Moi), Profesa John Kahamba alisema hiyo si mara ya kwanza kwa upandikizaji wa mikono kufanyika duniani kwani na tofauti kubwa na upandikizaji wa figo au ini.
    Jinsi unavyofanyika
    Profesa Kahamba alisema upasuaji huo unafanyika kwa kuhakiki mambo mbalimbali ikiwamo uwiano wa kundi la damu, uhai wa seli na misuli na mishipa midogo ya fahamu.
    “Upasuaji mkubwa hufanyika, pamoja na kuangalia uwiano wa damu lakini lazima jopo la madaktari wenye kazi tofauti lifanye kazi kwa pamoja. Kwa mfano, wanaounganisha misuli na mishipa midogomidogo na hata wale wa kuhakiki uhai wa seli,” alisema.
    Profesa Kahamba alisema kama upandikizaji wa figo unavyofanyika, kadhalika upandikizaji wa mikono unahitaji umakini wa muda.
    Anasema iwapo utachelewa kuunganisha mikono baada ya kuitoa, seli zake zinaweza kufa na kushindwa kufanya kazi zitakapopandikizwa kwenye mwili.
    “Katika hili, dawa za kuufanya mwili kukubali mikono hiyo lazima zipatikane kwa sababu mwili una tabia ya kukataa vitu vigeni,” alisema.
    Profesa Kahamba alisema upandikizaji wa aina hii ni mkubwa na unahitaji ushirikiano wa kada kadhaa za wataalamu wa afya na vitendea kazi sahihi na vya kisasa.

Previous
Next Post »