.

Ujambazi wa kuteka mabasi udhibitiwe

  • Katuni.
    Katika toleo letu la jana, tulichapisha habari kwenye ukurasa wa mbele yenye kichwa cha habari `Majambazi yateka mabasi saba Arusha. Yavua nguo abiria, yapora hadi viatu.'
    Habari hii ilieleza kwamba kundi la watu wanaosadikiwa kuwa majambazi, waliteka mabasi saba ya abiria yanayofanya safari zake kati ya Jiji la Arusha na Nairobi nchini Kenya Kenya na kupora mali na fedha ambavyo thamani yake haijafahamika.

    Tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia juzi katika eneo la Mbuga Nyeupe, Wilaya ya Longido mkoani Arusha baada ya watu hao kuweka mawe barabarani na kuwaamuru abiria wote kuteremka mmoja baada ya mwingine, kulala chini na kuwapekua kila kitu walichokuwa nacho.

    Dereva wa moja ya mabasi yaliyotekwa la Perfect Trans, Joseph John, alisema kuwa watu hao aliowakadiria kuwa wanafikia 50, walikuwa na silaha za jadi yakiwamo mashoka, mapanga na sime, waliteka mabasi hayo saa 8:00 usiku.

    Alisema waliteka magari yao yaliyokuwa yamefuatana na kuwapora kila kitu tena bila soni, wakalazimisha wanawake wavue nguo ili wachukue kila waliochoona kina thamani.

    Dereva huyo alisimulia kuwa yeye alikuwa wa kwanza kufika na basi eneo hilo na kukuta mawe yamepangwa katikati ya barabara.

    Alisema alisimamisha basi lake na kujaribu kuyakwepa mawe hayo, lakini moja ya majambazi hayo alimpiga jiwe usoni na hivyo kumfanya ashindwe kukimbia.

    Kwa mujibu wa dereva huyo, wakati majambazi hayo yakifanya unyama huo, baadhi yao hayakuficha sura zao.

    Aidha, dereva mwingine, Jabir Athumani, alisema  baadhi ya majambazi hayo yalikuwa yakiita kwa majina ya baadhi ya watu na kuwaamuru kutoa fedha walizokuwa nazo.

    Athumani ameviomba vyombo vya ulinzi na usalama vifuatilie tukio hilo kwa umakini wa hali ya juu ili kuwanasa wahusika.

    Kadhalika, alililitaka Jeshi la Polisi kurudisha magari ya doria katika barabara ya Arusha–Namanga ambayo yaliondolewa tangu Aprili, mwaka jana.

    Kwanza tunachukua fursa hii kuwapa pole abiria wote waliokumbwa na mkasa huu wa kusikitisha.

    Aidha, naso pia tunaungana na dereva aliyeliomba Jeshi la Polisi mkoani Arusha kuimarisha doria hasa maeneo ambayo ni sugu kwa ujambazi kama hilo na Mbuga Nyeupe wilayani Longido na kwingineko nchini.

    Tunachoshangaa ni kwamba polisi wanayafahamu fika maeneo hayo ambayo majambazi hupenda kuweka mitego na kupora abiria.

    Yapo maeneo mengi nchini yanafahamika kiasi kwamba hata polisi wakati mwingine huamua kuyasindikiza mabasi ya abiria kwa mitutu ya bunduki.

    Tunachoshangaa ni kwamba kama yanafahamika maeneo hayo, ni kwa nini Jeshi la Polisi lisiweke mitego na kuwaangamiza majambazi hayo badala ya kuyaacha yaendelee kutamba?

    Hatuamini kwamba majambazi yana uwezo zaidi kuizidi serikali isipokuwa hakuna dhamira ya dhati ya kuyateketeza.

    Tunaliomba Jeshi la Polisi liimarishe ulinzi  kwenye maeneo yote ambayo majambazi ni kama `yametangaza' kuwa ni yao ya kujidai na kuendelea kufuatilia nyendo zao kila kona ili kuondoa hofu kwa abiria wanaosafiri.
    CHANZO: NIPASHE

Previous
Next Post »