.

Kampeni za elimu bure zitasaidia kuboresha elimu yetu?


  • Kipindi cha kampeni za uchaguzi zinapokaribia, ni wakati muhimu sana kwa wananchi kuongeza umakini katika kusikiliza na kuamua ipi ni hoja au ahadi ya msingi kwa mustakbali wa nchi yetu.
    Ni hatari kama Watanzania tutakubali kuzugwa na hoja au ahadi za wagombea ambazo pengine kwa ufinyu wa upembuzi wetu, tutabaki kuziona na kuzishangilia kama hoja au ahadi mwanana kwa mustakbali wa nchi yetu, kumbe haziwezi kutusaidia kwenda mbele.
    Ni ukweli usiopingika kuwa, nchi yetu inahitaji mageuzi makubwa hasa kwenye sekta ya elimu ili tusonge mbele kwa mafanikio.
    Mwaka 2002 tulitangaziwa kuwa elimu ya msingi ni bure. Serikali iliahidi kutoa ruzuku ya Sh10,000 kwa kila mwanafunzi kuchukua nafasi ya mchango wa Upe. Ni kwa kiasi gani Serikali imezingatia na kutimiza ahadi yake hii?
    Ni kwa kiasi gani ruzuku ambayo imekuwa ikitolewa imesaidia kuifanya elimu ya msingi kuwa ya bure? Je, ni kwa kiasi gani ruzuku hii imemsaidia mzazi kupunguza gharama za kununua madaftari, kalamu, vitabu, usafiri na michango mingine ya shule?
    Yumkini ni wale tu wasioona wanaweza kuunga mkono ghiliba hizi za kutaka kurudisha nyuma juhudi za wananchi kuboresha huduma za shule zao kupitia michango yao ya hali na mali.
    Je, ni kipi hasa kinachangia Taifa letu kutoandikisha watoto wengi shule za sekondari? Ni karo, au gharama hizi zinazobebwa na wazazi?
    Tufute karo au tusaidie wazazi wasiojiweza kukidhi mahitaji ya watoto wao shuleni? Hili linawezekana kwa kuweka utaratibu maalumu wa wazazi kushiriki katika harakati za kutengeneza mazingira rafiki ya kufundishia na kujifunzia?
    Tujiulize hayaKuna mambo mengi tunatakiwa tujiulize kabla ya kukimbilia kauli hizi za wanasiasa. Ni kwa kiasi gani kwa mfano, kwa kuondoa karo kutasaidia kuongeza vitabu shuleni ikiwa hata Sh25,000 zinazotakiwa kutolewa kwa kila mwanafunzi wa sekondari hazifiki?
    Je, kuondoa karo kutasaidiaje walimu kupata mafunzo kazini, kupata vitendea kazi mfano chaki na madaftari ya maandalio ambayo Serikali ilishasahau kutoa kwa miaka mingi?
    Najua uamuzi wa kuifanya elimu ya sekondari kuwa bure itafuatiwa na ahadi ya Serikali kutoa ruzuku kufidia pengo. Ahadi za namna hii hazijaanza leo.
    Kwa kiasi gani Serikali imetimiza ahadi zake kila inapoanzisha mipango ya namna hii? Tumeshuhudia katika kipindi cha miaka 10 ya awamu ya kwanza na ya pili ya MMEM, hakuna hata mwaka mmoja Serikali imeweza kupeleka shuleni hiyo fedha iliyoahidi.
    - Mwananchi

Previous
Next Post »